Upendo wa Kweli

Kutoka Gospel Translations Swahili

Related resources
More By John MacArthur
Author Index
More About Loving Others
Topic Index
About this resource
English: True Love

© Ligonier Ministries

Share this
Our Mission
This resource is published by Gospel Translations, an online ministry that exists to make gospel-centered books and articles available for free in every nation and language.

Learn more (English).
How You Can Help
If you speak English well, you can volunteer with us as a translator.

Learn more (English).

By John MacArthur About Loving Others
Part of the series Article

Translation by May Adhiambo

Review You can help us improve by reviewing this translation for accuracy. Learn more (English).



“Unachohitaji ni upendo tu” ndivyo walivyoimba kikundi cha Beatles. Wangalikuwa wanaimba kuhusu upendo wa Mungu, taarifa hii ingekuwa na chembe cha ukweli. Lakini kitu kinachoitwa upendo katika utamaduni maarufu, si upendo halisi kamwe. Bali ni kejeli. Mbali na kuwa “chote unachohitaji” ni kitu ambacho wafaa kujiepusha nacho kabisa.

Mtume Paulo anaonyesha hoja hii dhahiri shahiri katika Waefeso 5:1-3. Anaandika, “Kwa hiyo, mfuateni Mungu kama watoto wapendwao, ,kiishi maisha ya upendo, kama vile Kristo alivyotupenda sisi akajitoa kwa ajili yetu kuwa sadaka yenye harufu nzuri na dhabihu kwa Mungu. Lakini uasherati, usitajwe miongoni mwenu, wala uchafu wa aina yo yote, wala tamaa, kwa sababu mambo haya hayastahili miongoni mwa watakatifu.”

Amri rahisi ya mstari wa pili (“mkiishi maisha ya upendo kama vile Kristo alivyotuenda sisi “) inajumuisha jukumu lote la kimaadili la mkristo. Kwani, upendo wa Mungu ndio kanuni moja kuu inayoeleza faradhi yote ya mkristo. Upendo wa aina hii ndiyo “chote unachohitaji” Warumi 13:8-10 inasema , “kwa maana yeye ampendaye mwenzake, ameitimiza sheria. Kwa kuwa amri….zinajumlishwa katika amri hii moja: ‘‘Mpende jirani yako kama nafsi yako.’’ Upendo haumfanyii jirani mabaya, kwa hivyo upendo ni matimizo ya amri ya Mungu. Wagalatia 5:14 inasisitiza ukweli huu ‘Kwa maana sheria yote hukamilika katika amri moja: “Mpende jirani yako kama nafsi yako.” Yesu vilevile alifunza ya kwamba Torati na manabii wanaegemea itikadi hizi mbili za kimsingi –amri kuu ya kwanza na ya pili (Matayo 22:38-40). Kwa maneno mengine, ”Upendo…..ndio unaofunga kila kitu pamoja katika amani kamilifu.” (Wakolosai 3 :14)

Paulo anapotuamrisha kutembea kwa upendo,mazingira yanatufunulia kuwa, kwa uzuri, anaongea kuhusu kuwa wafadhili,wenye kuhurumiana ninyi kwa ninyi, na wenye kusameheana (Waefeso 4 :32). Mfano wa upendo huu usio wa kibinafsi ni Kristo, ambaye alijitoa kafara ili kuwaokoa watu wake kutokana na dhambi zao. “Hakuna mtu mwenye upendo mkuu kuliko huu, mtu kuutoa uhai wake kwa ajili ya rafiki zake”(Yohana 15:13) Na “kama Mungu alitupenda sisi hivi, imetupasa na sisi kupendana “ (1 Yohana 4 :11).

Kwa maneno mengine, upendo wa kweli daima hujitoa kafara, hujitolea, huhurumia, hurehemu, hufadhili na husubiri. Hizi na sifa nyinginezo (angalia 1 Wakorinto 13:4-8) ndizo Bibilia inahusisha na upendo wa Mungu

Lakini katika Waefeso 5 tunaonyeshwa upande mwingine pia. Yeyote ambaye anawapenda wengine kwa kweli jinsi Kristo anavyotupenda lazima akatae kila aina ya upendo bandia . Mtume Paulo anavitaja vipengele fulani vya udanganyifu huu wa kishetani kama vile usherati, unajisi na tamaa. Kifungu kinaeleza zaidi : “Wala pasiwepo mazungumzo machafu ya aibu, au maneno ya upuzi au mzaha, ambayo hayafai, badala yake mshukuruni Mungu, Kwa habari ya mambo haya mjue hakika kwamba: Mwasherati, wala mtu mwovu, wala mwenye tamaa mbaya, mtu kama huyo ni mwabudu sanamu, ambaye kamwe hataurithi Ufalme wa Kristo na wa Mungu. Mtu ye yote na asiwadanganye kwa maneno matupu, kwa kuwa hasira ya Mungu huwaka kwa sababu ya mambo kama haya juu ya wale wasiomtii.Kwa hiyo, msishirikiane nao (mstari 4-7).

Katika kizazi chetu usherati mara nyingi huwa mbadala wa upendo. Paulo anatumia neno la kiyunani porneia linalojumuisha kila aina ya usherati. Utamaduni maarufu hautambui tofauti baina ya upendo wa kweli na ashiki ya kuzinzi. Lakini kuzini huku ni upotoshaji wa upendo wa kweli kwa sababu hutafuta kujinufaisha badala ya kunufaisha wengine.

Upotovu wa upendo wa kishetani wa namna nyingine ni unajisi. Hapa Paulo anatumia kigiriki akarthasia inayojumuisha kila aina ya aina ya uchafu na unajisi. Hasa, Paulo akilini anamaanisha uchafu, maneno ya upuzi au mzaha, ni sifa geni za usuhuba ovu. Usuhuba wa aina hii hauna uhusiano wowote na upendo wa kweli na mtume anadhihirisha haifai katika maisha ya kikristo.

Tamaa ni mfano mwingine wa upendo bandia inayotokana na nia batili ya kujinufaisha.Ni kinyume na mfano uliowekwa na Kristo alipokuwa “akijitoa kwa ajili yetu”(mstari 2) Katika mstari wa 5, Paulo anasawisha tamaa na kuabudu sanamu. Na mara nyingine tena, jambo hili halifai katika maisha ya kikristo, na kulingana na mstari wa 5, mtu afanyaye hivi “hataurithi ufalme wa Kristo na wa Mungu.”

Dhambi kama hizi, Paulo asema, “zisitajwe miongoni mwenu , kwa sababu mambo haya hayastahili miongoni mwa watakatifu.(mstari wa 3) Kwa wale wanaoyatenda haya, anatuambia, “ msishirikiane nao.”

Kwa maneno mengine , hatuonyeshi upendo halisi hadi pale ambapo hatuwezi kuvumilia upotovu wowote wa upendo.

Mazungumzo mengi ya siku hizi yanayohusu upendo hayazingatii kanuni hii. “Upendo ” umeelezwa upya kama uvumilivu mpana unaopuuza dhambi tena unaokumbatia wema na uovu kwa usawa. Huo si upendo bali ni kutojali.

Upendo wa Mungu hauwi hivyo. Kumbuka, dhihirisho kuu la upendo wa Mungu ni msalabani , pahali Kristo ‘alitupenda sisi akajitoa kwa ajili yetu kuwa sadaka yenye harufu nzuri na dhabihu kwa Mungu’ (mstari 2). Hivyo, Maandishi yanatueleza kuhusu upendo wa Mungu kutumia dhabihu na upatanisho - “Huu ndio upendo, si kwamba tulimpenda Mungu, bali Yeye alitupenda, akamtuma Mwanawe, ili Yeye awe dhabihu ya kipatanisho kwa ajili ya dhambi zetu.”(I Yohana 4:10). Kwa maneno mengine Kristo alijitoa kafara ili kugeuza hasira ya Mungu aliyekwazwa . Mbali na kuondoa dhambi zetu kwa uvumilivu, Mungu alimtoa mwanawe kama sadaka ya dhambi, kukidhi hasira yake Mwenyewe na kuleta haki katika wokovu wa wenye dhambi.

Hicho ndicho kiini cha injili. Mungu anaonyesha upendo wake kwa njia ambayo inadumisha utakatifu, haki na uongofu bila kurudi nyuma. Upendo wa kweli “haufurahii mabaya bali hufurahi pamoja na kweli” (1 Wakorinto 13:6). Wito wetu ni kutembea kwa upendo wa aina hii.Ni upendo ambao kwanza ni takatifu kisha wenye amani.